0
>Rais Jakaya Kikwete amesema idadi ya wanachama wa CCM waliojitokeza kuwania urais ni kubwa,



kutoa mgombea urais, ulipangwa kufanyika kesho na keshokutwa, lakini taarifa zilizopatikana baadaye zilisema utafanyika kwa siku moja tu ya kesho.

Nape alipotafutwa mara mbili kwa nyakati tofauti jana, majibu yake yalikuwa mafupi; “ratiba niliyotoa ndiyo hiyohiyo, ifuateni kama mnataka kuandika”.

Alipotafutwa jioni baada ya kuenea tetesi kwamba vikao vyote vitafanyika leo, hakupokea simu lakini alituma ujumbe mfupi wa maandishi ukisema: “Siwezi kuongea sasa… Samahani nipo kikaoni, tuma meseji”. Lakini hata alivyotumiwa ujumbe hakujibu.

Baadhi ya wajumbe wa Kamati Kuu walipoulizwa kikao chao kingefanyika lini, walisema hawakuwa na taarifa na kwamba na wao walikuwa wanasubiri kupewa taarifa.

Mmoja wa wajumbe wa NEC aliyekuwa akizunguka kwenye ofisi za makao makuu ya CCM, huku akionyesha amechoka, alisema: “Hapa nilipo hata sifahamu tutafanya lini kikao, nipo tu nazunguka hapa.”

Giza hilo ambalo limewakumba wagombea na wajumbe wa vikao, pia limesababisha kuenea kwa tetesi dhidi ya hatima za wagombea na kutoa fursa kwa wajumbe wenyewe kuzodoana.

“Mgombea wako keshamalizwa, kikao cha kamati ya maadili kimeshamkata,” ni miongoni mwa tetesi walizokuwa wakirushana roho wajumbe wa vikao vya CCM, ingawa taarifa za uhakika ni kuwa kikao hicho kilikuwa hakijafanyika.

Wengine waliokuwa na uelewa mpana walijibu kwamba vikao havijafanyika, hivyo kuhoji mgombea angekatwa na kikao gani.

Taarifa nyingine zilidai kuwa Kamati ya Usalama na Maadili ina dozi za baadhi ya wagombea maarufu na kwamba alama za ufaulu kwenye kamati hiyo zimewamaliza wengi.

Wagombea wanena

Pamoja na ratiba ya vikao hivyo kubadilikabadilika, makada waliojitokeza kuwania urais kwa tiketi ya CCM hawakuonekana kusumbuliwa na jambo hilo.

Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja alisema hana tatizo na kuchelewa kwa vikao hivyo kwa kuwa vina ratiba zake na maandalizi yapo ndani ya ratiba. Alisema viongozi wataendelea kutoa miongozo na anaamini msemaji wa chama ataendelea kuujulisha umma kinachoendelea.

Mgombea mwingine, Dk Hamis Kigwangalla alisema hakuwa na taarifa rasmi za kutofanyika kwa vikao kama vilivyopangwa, lakini akasema hilo halikuwa na madhara kwa wagombea na anaona sababu za kufanya hivyo ni kupunguza presha.

“Naamini vikao vyote vitakaa na chama chetu kuvisogeza mbele ni jambo la kawaida tumeshazoea. Nikiwa mmoja wa wagombea, sina shaka wala wasiwasi wowote, ratiba iliyopangwa ya vikao hivi imekutana na jambo kubwa.

Rais anatakiwa kuvunja Bunge na baadhi ya wajumbe watahudhuria shughuli hiyo, hivyo lazima visogezwe mbele,” alisema  mgombea mwingine January Makamba.

Mwalimu Banda Sonoko alisema kila kitu ni maandalizi hivyo anaamini kesho watakuwa wamepata mgombea, kwani vikao hivyo vimeingiliwa na mambo mengi, ndiyo maana vimesogezwa.

“Sina tatizo lolote, natambua mwenyekiti wangu pia ni Rais ana shughuli nyingi. Hili ni jambo zito, wahusika wanahitaji wasaa ili wasije kutupatia mgombea ambaye hafai, sidhuriki na hii chelewa chelewa, nitavumilia na kujigharimia kwa muda wote lakini tupate mgombea safi,” alisema Balozi Ali Karume.

Mjumbe wa kamati ya kampeni ya Lowassa, Hussein Bashe alisema hili siyo jambo la ajabu, bali ni kawaida kutokana na maelekezo ya chama vikao ni mpaka Julai 12.

“Kuahirisha vikao vya Kamati ya Maadili, Kamati Kuu na NEC siyo jambo la kutilia shaka,” alisema.

Msemaji wa Stephen Wasira, Masyaga Matinyi alisema anaamini kanuni, taratibu na katiba ya chama vitaheshimiwa hivyo mchakato utakuwa wa haki.

“(Wasira) Anaamini vikao vitafanyika kwa mujibu wa taratibu zilizopangwa, hivyo kuahirishwa huko hakuwezi kuvuruga mchakato,” alisema Matinyi.

Kada mwingine kwenye mbio hizo, Elidephonce Bilohe alisema anamwomba Mungu ili kuahirishwa kwa vikao hivyo kumpe neema kwa jina lake kupitishwa kuwa mgombea urais wa chama hicho.

“Jana (juzi) nilikwenda ofisi za CCM nikakutana na ofisa wa ngazi ya juu ya chama akaniambia kama tukihitajika na kikao chochote tutaitwa. Basi nikaondoka, nipo hapa nyumbani namwomba Mungu anisaidie niweze kuipata nafasi hii,” alisema Bihole.

Boniface Ndengo alisema kuahirishwa kwa vikao hivyo vya mchujo wa wagombea anaona hakuna tatizo.

“Nilishafanya sehemu yangu niliyotakiwa, sioni kama kuna usumbufu wowote,” alisema Ndengo.

Leonce Mulende alisema suala hilo halimpi matatizo ya kisaikolojia kwa sababu limewekewa programu za msingi, hivyo anafikiri watafikia hatima vizuri.

Balozi Patrick Chokala alisema: “Wenye shughuli zao ndiyo wanajua sababu za kuchelewa, wacha tusubiri watamaliza tu.”

Source MWANANCHI
Imeandikwa na Midraj Ibrahim, Noor Shija, Sharon Sauwa (Dodoma) na Suzan Mwillo (Dar).

Post a Comment

 
Top